UDOSO YAJA NA MKAKATI MPYA: WANAFUNZI UDOM KUSAINI PESA HATA KAMA HAWAJALIPA ADA.


Serikali ya wanafunzi chuo kikuu cha Dodom (UDOSO) imewasilisha mkakati mpya kwenye suala la kusaini pesa za kujikimu kwa wakurufunzi wa chuo kikuu cha Dodoma na koleji zake. Mahenga imemtafuta na kuzungumza naye kwa njia ya simu kulitolea ufafanuzi suala hili leo terehe 23 Oktoba majira ya jioni.

Akizungumza kwa niaba ya UDOSO, rais wa shirikisho chuo kikuu cha Dodoma Bw. Bruno Julian Kayoza amethibitisha kuwa, tayari wamefanya mazungumzo na menejimenti ya chuo juu ya mpango huo.

Bw. Bruno amesema kuwa, karibu asilimia 70 ya wanafunzi wanategemea pesa za kujikimu ili kulipa ada zao na michango mingine ya chuo. "...unajua kaka asikwambie mtu, karibu wanafunzi wote wanategemea pesa hiyo ya kujikimu ili kulipa ada na michango minge, niseme tu asilimia 70 ya wanafunzi...". Amesema.

Aidha, mkakati huo utakuja katika makubaliano maalumu ya ujazaji fomu za makato ya moja kwa moja (automatic reduction form) ambayo mkurufunzi ataijaza kubainisha ni kiasi gani anadaiwa ili pesa hiyo ikiingia deni litakatwa moja kwa moja. "...tumeongea na menejimenti ya chuo na wametupa mbinu hiyo, ambayo nafikiri itawasaidia wengi kuendelea na masomo yao bila kero ya aina yoyote.." Bruno amesema.

Sanjari na hilo, Bw. Bruno ametanguliza kuomba radhi kwa mapungufu yote ambayo yalijitokeza hapa katikati na serikali yake kuonekana haikufanya kazi, lakini matatizo mengine yalisababishwa na serikali, hivyo yalikuwa nje ya uwezo wao. Bw. Bruno pia amewataka wakurufunzi kuwa na moyo wa uvumilivu kwani kipindi hiki ni cha mpito na amehimiza kuendelea kumpa ushirikiano katika kero mbalimbali zinazowakabiri wakurufunzi.

Chapisha Maoni

0 Maoni