Clinton: Bifu langu na Putin limenifanya nikose urais

Baada ya kimya kirefu tangu ashindwe kupata nafasi ya Urais nchini Marekani, hatimaye aliyekuwa mgombea nafasi hiyo Hillary Clinton amejitokeza na kudai kwamba ugomvi binafsi uliokuwepo kati yake na Rais Vladmir Putin wa Urusi umechangia sana kumkosesha nafasi hiyo muhimu.
Clinton ameeleza hayo wakati huu kukiwa na mzozo mpya kati ya serikali ya Marekani na Urusi juu ya kuwepo taarifa za kiintelijensia kwamba Rais Putin alidhamini kitengo cha udukuzi ili kiingilie na kuvuruga uchaguzi mkuu wa nchi hiyo, na tayari Rais Obama ametoa agizo la kufanyika uchunguzi na kusema kuwa serikali yake itachukua hatua kali dhidi ya Urusi.
Katika mahajiano aliyofanya siku ya Alhamisi usiku, Clinton amesema kuwa Rais Putin alikuwa akijaribu hata kuzivuruga kampeni zake ilimradi tu kumharibia njia yake kutokana na “Ugomvi Binafsi.” 
“Putin alikuwa akinilaumu kwa kuwaambia ukweli raia wa Urusi kuwa walidhulumiwa haki yao, vitu ambavyo vinafanana na kile alichoamua kukifanya yeye kwa kuingia uchaguzi wetu na kuharibu kila kitu kama njia ya kulipa kisasi,”amesema Hillary.
Clinton amefananisha kilichotokea kwake ni kile kilichowapata Warusi kwenye uchaguzi uliovurugwa na usio wa kidemokrasia kwenye bunge la Urusi mwaka 2011.
Mgombea huyo amesema ana uhakika angeshinda uchaguzi kama tu Putin asingeingilia na kuvuruga pia aliendeleza lawama zake kwa Mkurugenzi wa shirika la kijasusi la nchi hiyo FBI, James Comey kwa kushupalia taarifa za uchunguzi wa email zake binafsi kuwa zilipunguza kura zake.

Chapisha Maoni

0 Maoni