Uwanjani: Aveva amvuta 'Mbuyu Twite' Simba

RAIS wa klabu ya Simba Evans Aveva yupo kwenye mazungumzo na kiungo mkabaji aliyemaliza mkataba wa kuitumikia Yanga rai wa DR Congo Mbuyu Twite, ili kumsajili kwa ajili ya kuwaongezea nguvu kwenye mzunguko wa pili wa ligi ya Vodacom unaotarajiwa kuanza Desemba 17.

Aveva amesema , wanamuhitaji Twite, kutokana na uwezo aliokuwa nao na wanaamini atawasaidia kwa siku za karibuni kabla ya mchezaji huyo kuamua kustaafu.

“Nikweli tupo kwenye mazungumzo na Twite, bado hatujaafikiana baadhi ya mambo kingine kilichochelewesha tulikuwa tunamsubiri kocha ili aweze kuidhinisha usajili wake ambao kama utafanikiwa atatusaidia kucheza kwenye safu ya ulinzi kutokana na uzoefu aliokuwa nao,”amesema Aveva.

Kiongozi huyo amesema Mbuyu pamoja na umri mkubwa aliokuwa nao lakini ni mchezaji mwenye uwezo mkubwa na amekuwa na nidhamu ndani na nje ya uwanja hivyo wao wanaamini anayonafasi kwenye kikosi chao ambacho kinapigania ubingwa wa ligi ya Vodacom msimu huu.

Amesema wanamapungufu kwenye nafasi za kiungo mkabaji namba sita na beki wa kulia mchezaji huyo anaweza kuwa mtu sahihi kwasababu anazimudu vyema nafasi hizo na ndiyo maana wanataka kumchukua .

“Kwenye beki wa kulia tunaye Jamvier Bukungu raia wa DR Congo na kati tunaye nahodha Jonas Mkude pekee sasa Twite nafasi zote hizi anazimudu ndiyo maana tunataka kumchukua ili awe msaidizi katika nafasi yoyote kati ya hizo kama kutatokea mmoja wao kuwa majeruhi au kitu kingine,”amesema.

Aveva amesema kwa muda mrefu walikuwa wakimuhitaji mlinzi huyo lakini walishindwa kumchukua kutokana na kuwa na mikataba na klabu yake ya Yanga.

Endapo dili hilo litakamilika itakuwa ni mara ya pili kwa Twite anasajiliwa na Simba, mara ya kwanza alisajiliwa timu hiyo lakini alishindwa kuichezea, licha ya kutambulishwa sikuchache alitua Yanga wakitumia mapungufu machache yaliyokuwepo kweye fomu za usajili uliofanywa na Rais wa wakati huo Ismail Aden Rage.

Chapisha Maoni

0 Maoni