Shahidi kesi ya Tundu Lissu abanwa tafsiri ya neno 'Dikteta uchwara'

Tafsiri ya maneno “dikteta uchwara” yanayodaiwa kutamkwa na Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu kuhusu uminywaji wa demokrasia nchini, jana ilizua mjadala mahakamani baina ya mawakili wa pande zote mbili.


Wakili Peter Kibatala anayemtetea Lissu katika kesi ya uchochezi, alimbana kwa maswali shahidi E4128 D/Staff Sajenti Ndege aeleze tafsiri halisi ya kauli hiyo na kwa nini walidhani ni uchochezi.

Ni baada ya Ndege akiongozwa na Wakili wa Serikali, Salum Mohammed kumweleza Hakimu Mkazi Mkuu, Godfrey Mwambapa kuwa maneno yaliyotamkwa na Lissu aliona yanaashiria uchochezi na kuleta ushawishi kwa Watanzania kupinga mamlaka.

“Kwa kuwa Lissu ni kiongozi aliyechaguliwa na wananchi pia alikuwa na ushawishi kwa wananchi na wakamchagua kuwa mbunge wao, alipotamka maneno hayo alikuwa anaashiria ushawishi kwa watu kupinga mamlaka ya Serikali,” alidai.

Aliongeza, “Hivyo, mimi na kiongozi wangu Kimweli tulishauriana na kuwa hiki alichokifanya kinaenda kinyume na mwenendo wa sheria za nchi, hivyo tukalazimika kutoa taarifa polisi kati.”

Baada ya kueleza hayo, Kibatala alimuhoji, alimsikia Lissu akisema nini? Ndege alidai kuwa alimsikia akitamka, ‘Mamlaka ya Serikali mbovu ya kidikteta uchwara inapaswa kupingwa kwa nguvu zote na kila Mtanzania” na kwamba “utawala wa nguvu ukiachwa unaweza kupelekea nchi kuingia kwenye giza nene”.

Baada ya kueleza hayo, Kibatala alimuuliza shahidi, kama kwa maoni yake mtazamo wa Tanzania kupingana na utawala dhalimu wa Afrika Kusini ulikuwa siyo sahihi? Shahidi huyo alidai kuwa ulikuwa sahihi.

Kibatala: “Ni sahihi uongozi wa Tanzania utuhamasishe watu wake kupinga udhalimu huo na tulikubaliana nao?”

Shahidi: Ni sahihi.

Kibatala: Ni kweli kwamba tulipigana vita na Idd Amin kutokana na utawala wake wa udikteta?

Shahidi: Ni sahihi.

Kibatala: Ni sahihi wakati wa vita ya Uganda,(Mwalimu) Nyerere alihamasisha kila Mtanzania kupinga utawala wa kidikteta wa Idd Amin?

Shahidi: Ni sahihi.

Kibatala: Lissu aliposema mamlaka ya Serikali mbovu ya kidikteta uchwara inapaswa kupingwa kwa nguvu zote na kila Mtanzania aliitaja ni Serikali gani?

Shahidi: Hakuitaja ni Serikali ipi.

Kibatala: Aliposema utawala wa nguvu ukiachwa unaweza kupelekea nchi kuingia kwenye giza nene, alitaja ni Serikali gani hiyo?

Shahidi: Hakutaja jina la nchi.

Kibatala: Ni kweli kwamba kilichokufanya wewe na kiongozi wako, Mrakibu Msaidizi wa Polisi (ASP) Kimweli kuripoti Polisi Kati ilikuwa ni tafsiri yenu ya maneno hayo, inamaanisha Tanzania?

Shahidi: Ndiyo

Kibatala: Kwa kuwa nyie ndiyo mlikereketwa na tukio hilo, siku hiyo Mahakama ya Kisutu kulikuwa hakuna askari polisi wengine zaidi yenu?

Shahidi: Hapana.

Shahidi alidai kuwa yeye na Kimweli walitoa taarifa za tukio hilo kwa ZCO, Camilius Wambura na kuwa yeye aliandika maelezo kama shahidi aliyeshuhudia tukio yeye mwenyewe na maelezo hayo hayakushuhudiwa na mtu mwingine yoyote na aliyakabidhi kwa afande Kimweli.

Kabla ya mahojiano hayo na Kibatala, Ndege aliiambia mahakama kuwa maneno hayo aliona yanaashiria uchochezi na kuleta ushawishi kwa Watanzania kupinga mamlaka. Kesi hiyo imeahirishwa hadi Januari 21,2016 kwa ajili ya kuendelea kwa ushahidi wa mashahidi wa upande wa mashtaka.

Katika kesi hiyo, Lissu ambaye pia ni Mnadhimu wa Kambi ya Upinzani bungeni na Mwanasheria Mkuu wa Chadema anadaiwa kutoa kauli za uchochezi dhidi ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano.

Anadaiwa kuwa Juni 28, mwaka huu, akiwa katika viwanja vya Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu,alitoa kauli za uchochezi kuwa, “Mamlaka ya Serikali mbovu ni ya kidikteta uchwara inahitaji kupingwa na kila Mtanzania kwa nguvu zote, “huyu diktekta uchwara lazima apingwe kila sehemu”. Kama uongozi utafanywa na utawala wa kijinga nchi inaingia ndani ya giza nene.’’

Chapisha Maoni

0 Maoni