Askofu: Watanzania tumuunge mkono rais Magufuli

WAKRISTO nchini wameaswa kuunga mkono juhudi za Rais John Magufuli za kupiga vita ubinafsi ili kujenga nchi yenye upendo, amani na maendeleo.
Mwito huo umetolewa na Askofu wa Kanisa la Moravian, Jimbo la Mashariki na Pwani Tanzania, Emmaus Bandekile Mwamakula jana katika salamu zake kwa wakristo za Sikukuu ya Krismasi na Mwaka Mpya.
“Tunaposherehekea sikukuu ya Krismasi hatuna budi kukumbuka maana halisi ya Krismasi. Biblia inafundisha kuwa Yesu Kristo aliamua kuacha utukufu wote aliokuwa nao mbinguni pale alipozaliwa sehemu ya kulishia ng’ombe ili awatumikie na kuwakomboa wanadamu,” alisema Askofu Mwamakula.
Alisema tukio la kumbukizi ya kuzaliwa Yesu Kristo linawakumbusha Wakristo kuacha ubinafsi na kwani hakuna jamii yoyote iliyofanikiwa popote duniani kama inaendeleza ubinafsi.
Askofu Mwamakula alisema vita dhidi ya ubinafsi inayopigwa kwa nguvu zote na Rais Magufuli, inapaswa kuungwa mkono kwani ubinafsi ni adui wa haki, upendo, umoja, amani na maendeleo.
"Ubinafsi unafanya hospitali zinakosa dawa na huduma muhimu na kusababisha watu ambao wangekuwa wazalishaji mali kupoteza maisha kwasababu tu watu wachache wametumia pesa zilizotakiwa kutumika kuwatibia,” alisema askofu huyo.
Alisema Rais Magufuli ametambua madhara ya ubinafsi ndio maana ameanzisha vita alivyovipa jina la “Kutumbua Majipu” hivyo anapaswa kuungwa mkono na kupongezwa.
Aliwasihi Watanzania wote kuungana kwa kuwa vita hivyo havina dini, kabila, itikadi, jinsia, umri wala rangi na kuongeza kuwa kama jamii inahitaji demokrasia ya kweli, ni lazima kupiga vita ubinafsi.

Chapisha Maoni

0 Maoni