Makala; Uhuru wa mtu unatokana na nini?



Ili kupata majibu ni uhuru unaanzia wapi, nadhani ni vema tukarejea tena kwa hadithi ya kweli ya mtaalamu wa saikolojia na tabia za binadamu Viktor Frankl.
Frankl alikuzwa kifikra kwa kutegemea mafunzo ya katika somo la saikolojia toka kwa nguli Sigmund Freud. Nadharia za Freud zimejengwa katika msingi ya kuwa tabia ya mwanadamu inajengwa au kuchongwa na hali ya nje ya mazingira yanayomzunguka kwa asilimia zaidi ya 70. Kwa tafsiri nyingine haiba (personality) na tabia (character) ya mtu zitaathiriwa sana na hali ya nje au mazingira yanayomzunguka.
Kwa msingi wa nadharia hiyo, ukomo na mfumo wa maisha ya mtu huwa mara nyingi huwa inafungwa kutokana na hali inayomzunguka na inakuwa ngumu kujikomboa kutoka hapo na kuishi maisha nje ya mfumo uliokuzunguka.
Frankl alikuwa daktari bingwa wa afya ya akili na raia Austria wenye asili ya Kiyahudi alikuwa kafungwa gerezani huko Ujerumani nyakati za dikteta na mfashisti Adolf Hitler. Akiwa gerezani alipitia maisha ya mateso na msoto ambao hayakujali kabisa utu. Kupitia mateso hayo, baba yake, mama yake na mkewe waliaga dunia kufuatia zoezi la kutumbukizwa katika tanuru la moto wa gesi.
Ni dada yake tu na yeye ndiyo walipona. Frankl alipata mateso na kufikia wakati wa kutojua uwezekano wa kuiona kesho na maisha yake yake yatakuwaje. Kutokana na hayo mara kwa mara alikuwa na maswali mawili, je anaweza “kuokoka” na tanuru la gesi na ataishi chini ya mateso hayo mpaka lini?.
Siku moja akiwa pekee na utupu katika chumba, akajiuliza swali, uhuru wa mtu ni kitu gani hasa? Ni uhuru upi ambao askari magereza wa kinazi hawawezi kumwondolea kabisa hata ikiwa gerezani katika maisha magumu?
Kumbuka, askari wale walikuwa wanadhibiti mazingira yake (they had control over his environment) na kumtendea chochote chenye kuleta maumivu katika mwili wake.
Pamoja na changamoto hizo za mateso, Frankl alikuwa anafahamu kuwa, utambulisho wake hauwezi kupotea. Alijiona kuwa na uhuru wa kufikiri chochote kile mbali na mateso anayopata.
Yeye kama msomi aliamua kuanza kupiga picha mpya na kupata taswira tofauti katika akili yake.
Kati ya msoto na mateso, alianza kujiona siku moja atakuwa darasani anafundisha baada ya kutoka “segerea ya huko”.
Baada kuifunza akili yake na mwendelezo wa nidhamu ya hali ya juu kwa jinsi anavyotakiwa kufikiri tofauti, akili yake, mihemko (emotions), mwenendo wake gerezani na namna ya kuhusiana na wanyapara ilibadilika.
Mara tabia yake ikabadilika na kukawa na uhuru wa mazungumzo ya kati yake na wanyapara wanaomtesa. Kwa namna flani alianza kuwajengea uwezo wale wanyapara wale ili wajitambue na kujua kusudi la maisha yao (he empowered his captors to know the sense of lpurpose in their lives).
Frankl alitumia dhana ya utajiri alionao mtu akitambua kusudi la yeye kuishi na faida ya kutoa mchango wake kwa kuwasaidia wengine kuishi maisha ya uhuru na furaha.
Kukatisha hadithi hii ya kweli, baada ya miaka 3 Viktor Frankil alikuwa mtu huru nje ya gereza na aliweza kuwa mmoja wa wasemaji wa kujengea watu uwezo (motivational speakers). Amendika vitabu kadhaa na moja ya vitabu alivyouza sana kinaitwa Man's Search for Meaning (mtu kutafuta maana ya maisha)
Naomba Watanzania tujifunze kutoka kwa Frankl. Kiuhalisia Tanzania inapitia katika changamoto kubwa ya kimtazamo kwa sasa. Ukisoma magazeti, ukisikiza mijadala ya redioni, vijiweni na kwenye mitandao ya kijamii, unaweza kuvurungwa sana kwa namna ambavyo lawama na manung’uniko ni makubwa kuliko habari zenye matumaini.
Najaribu kujiuliza, mzee Nelson Mandela aliekaa gerezani miaka 27 katika chumba kidogo, kitanda chake kikiwa ni sakafu, choo chake kikiwa ni ndoo, akifanyishwa kazi ngumu ya kuponda kokoto. Mandela aliruhusiwa kuetembelewa na mtu mmoja tu garezani kwa mwaka, na kuwa na mazungumzo yasiyozidi dakika 30 tu.
Kimsingi, Frankl na Mandela ilitakiwa “wavunjike” kiakili kutokana na msoto walioupata kutoka gerezani mmoja akiwa chini ya wanazi na mwingine chini ya makaburu. Msingi mkubwa wa selo za wafungwa kama Mandela na Frankl ni ilikuwa kuwavuruga kiakili na ndiyo maana wafungwa wengi wakitoka gerezani huwa wamekata tamaa. Baadhi huwa wanajihusisha tena na uhalifu ili warejee gerezani.
Najaribu kujiuliza, ni Watanzania wangapi wanatambua maana ya kuishi hatima (sense of purpose towards destiny) bila kujali changamoto au ugumu wa mazingira yanayomzunguka au habari hasi anayoisikia?
Saulos Tarseus mwanafalsafa na msomi wa sheria kule mashariki ya kati wakati mmoja akiwahusia wanafunzi wake kwa barua, aliwaambia “...badilikeni kwa kufanya upya akili zenu...” (be transformed by renewal of your mind). Akili ya mtu ni kitu cha msingi sana ili afike kule anakotaka kwenda bila kujali anapitia ugumu gani katika wakati aliopo kwa sasa. Je, Watanzania, kila mtu kwa nafsi yake, anajua anataka kwenda wapi ndani ya miaka kadhaa?
Vikwanzo unavyopitia ni vikali kama vifungo na mateso ya Frankl au Mandela? Unafikiria na kujiona uko nje ya gereza na kuwa Rais wa nchi yako au mkurungenzi wa taasisi au kampuni lako? Mandela alifikia ndoto yake ya kuwa rais wan chi yake. Frankl aliweza tena kuwa mhadhiri. Mpaka lini lawama zielekezwa kwa bosi, mazingira, wazazi au hali ya kisiasa ilivyo kwa sasa?
Muamuzi wa kuifanya kesho yako iwe bora na njema kwako, familia yako na watu wanaokuzunguka inakutegemea sana wewe kwa kuamua kwa usahihi. Msingi wa maamuzi bora huanzia pale mtu anapopata taarifa sahihi hali kadhalika kuzungukwa na watu sahihi. Lakini hata kama hakuna watu watu sahihi, uamuzi wa kufikia maisha yenye kuongeza thamani kwa wengine huanzia kwako.
Mtu moja alipata kusema “The same boiling water that softens the potato hardens the egg. It's about what you're made of, not the circumstances”
Maji yale yale yanayochemka ambayo kiazi kinalainika ndiyo hayahayo ambayo yanafanya yai liwe gumu. Inategemea nini kimekutengeneza na si mazingira au hali ya nje iliyokuzunguka.
Nawatakiwa Heri za Krismas na sherehe za kupokea mwaka 2017.

Chapisha Maoni

0 Maoni