Msuva anawasubiria Yanga tu, Atimke zake

KIUNGO mshambuliaji wa timu ya Yanga, Simon Msuva, ameeleza kuwa anasubiri baraka kutoka kwa uongozi wa klabu hiyo wamruhusu akatafute maisha kwingine, ili aweze kusukuma gurudumu la maisha yake.

Msuva amethibitisha kutakiwa na klabu tatu kubwa zinazocheza Ligi Kuu nchini Misri, ambazo zimekuwa na upinzani mkali katika ligi hiyo.


Mchezaji huyo ambaye hivi karibuni alipewa tuzo ya mfungaji bora kwa kufunga mabao 14 katika Ligi Kuu Tanzania Bara msimu uliopita, huenda akafikia lengo lake hilo kutokana na mkataba wake na Yanga kuelekea  ukingoni.

Mei 12, mwaka huu klabu ya Al Ettihad ya Misri ilifanya mazungumzo na kiungo huyo, kabla klabu kongwe ya Zamalek nayo ikitokea nchini humo kuingilia kati ikitaka huduma ya mshambuliaji huyo.

Akizungumza na MTANZANIA jana, Msuva alisema hawezi kufanya uamuzi wowote kabla ya klabu yake ya Yanga haijaamua, kwa sababu bado yupo chini ya uongozi wa klabu hiyo, hivyo uamuzi wa mwisho unatarajiwa kutoka kwao.

“Lengo langu msimu ujao niwe kwenye klabu nyingine nje ya Tanzania, kwa kuwa tayari kuna klabu tatu ambazo zimeonesha nia ya kuhitaji huduma yangu.

“Lakini kama ambavyo utaratibu unavyokuwa, mimi bado niko chini ya uongozi wa klabu ya Yanga, si vema nikafanya uamuzi bila kuheshimu mamlaka inayoniongoza,” alisema Msuva.

Alieleza tayari uongozi wa Yanga una taarifa juu ya kuondoka kwake na ana imani kubwa ya kupata ruhusa kutoka kwa uongozi huo ili akajaribu maisha kwingine.

Mbali na klabu hizo za Misri, Mamelod Sundown inayoshiriki Ligi Kuu nchini Afrika Kusini, pia imeonyesha nia ya kumuhitaji mchezaji huyo.

Kama Yanga itamruhusu Msuva, basi atakuwa ni mmoja wa wachezaji wachache waliopata ruhusa kucheza nje, kutokana na klabu hiyo kuwa na kasumba ya kutoruhusu wachezaji kununuliwa na timu nyingine.

Chapisha Maoni

0 Maoni