Mafunzo yasababisha diwani kubaini hasara ya shilingi 1.8 bilioni


Na. Ahmad Mmow.
LICHA ya kumuongezea uwezo wa kutumbua wajibu na majukumu yake kutokana na mafunzo ya uimarishaji wa mifumo ya sekta za umma. Diwani wa kata ya Nangowe katika halmashauri ya wilaya ya Nachingwea, Ally Chitanda amekiri kuwa mafunzo hayo ambayo yaliandaliwa na mradi wa uimarishaji wa mifumo ya sekta za umma (PS3)yamemuwezesha kubaini kuwa halmashauri yake ilikosa shilingi 1.8 bilioni kutokana na ushuru wa zao la korosho kwa msimu wa 2016/2017.


Akizungumza na blogi hii baada ya kufungwa mafunzo hayo ya siku mbili yaliyofanyika katika kumbi za mikutano za Sea view na Doble M, katika manispaa ya Lindi. Chitanda  aliyekiri kuwa mafunzo yamewajengea uwezo wa kuyatambua majumu na wajibu wao, yamemuwezesha kubaini kuwa halmashauri ya wilaya ya Nachingwea ingeweza kupata takribani shilingi 3.00 bilioni badala ya shilingi 1.2 bilioni zilizotokana na ushuru wa zao la korosho.

Iwapo wangekuwa wamepata mafunzo hayo mapema. Alisema katika msimu wa 2016/2017 katika halmashauri hiyo zilinunuliwa korosho zenye uzito wa tani 20, 000. Hata hivyo korosho hizo zililipiwa ushuru kwa kuzingatia bei elekezi iliyotangazwa na serikali kupitia bodi ya korosho, ambayo ilikuwa ni shilingi 1, 300/= kwa kila kilo moja kwa daraja la kwanza na shilingi 1, 000/= kwa daraja la pili. "Kutojua kwetu kulisababisha tupate asilimia tano ya bei iliyotangazwa na bodi ya korosho, ambayo ni shilingi 60  kwa kila kilo moja.

Kumbe tulitakiwa tuchukue ushuru kutokana na bei iliyouziwa sokoni.," alisema   Chitanda. Alibainisha kwamba katika msimu uliopita korosho zilinunuliwa kwa watani wa shilingi 3, 000 kwa kila kilo moja.

Hivyo Kulikuwa na uwezekano wa kupata shilingi 3.00 bilioni iwapo kila kilo ingelipiwa ushuru wa shilingi 150/=.Hata hivyo halmashauri ilipata shilingi 1.2   bilioni. Alisema fedha hizo zingesaidia kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo.

Huku  akiweka wazi kwamba fedha za ushuru wa mazao hazikatwi kutoka kwenye fedha za wakulima bali wanunuzi. Aliongeza kusema baada ya kupata mafunzo hayo, hali hiyo haitajirudia. "Aya mafunzo yamechelewa, ilitakiwa baada yatkuchaguliwa  tu, tungepewa. Wengi wetu hatukuwa na uzoefu, wale wachache waliokuwa na upeo mkubwa kwenye masuala aya wakihoji walikuwa wanaonekana wakorofi na walikuwa wanazomewa.

Sasa kila mtu amesikia na ameelewa, "alisema kwa kujiamini Chitanda. Mafunzo hayo ya siku mbili kwa madiwani yaliandaliwa na mradi wa uimarishaji wa mifumo ya sekta za umma kwa ufadhili wa shirika la misaada la watu wa Marekani (USAID). Ambapo mafunzo yalitolewa na chuo cha serikali za mitaa, Hombolo. 

Chapisha Maoni

0 Maoni