Afisa TRA apandishwa kizimbani


Ofisa Msaidizi wa Kodi wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Joyce Amon amefikishwa katika Mahakama ya Wilaya ya Ilala akikabiliwa na shtaka la kushawishi rushwa.

Wakili wa Serikali, Sophia Nyanda alisema jana  Ijumaa Machi 9, 2018  mbele ya Hakimu Mkazi  Adelf Sachore kuwa  Desemba 12, 2017  katika eneo la Gerezani Kariakoo Wilaya ya Ilala mshtakiwa huyo akiwa mwajiriwa wa TRA kama Ofisa Msaidizi wa Kodi alishawishi rushwa ya Sh800,000 kutoka kwa Antelo Sanga ili asiweze kumwandikia cheti cha faini cha  Kodi  ya Ongezeko la Thamani  (VAT).

Katika shtaka la pili, mwanafunzi  Lilian  Wilson (23) naye anakabiliwa na shtaka la kusaidia kutenda kosa hilo.

Wakili Nyanda alidai Desemba 13,2017 katika Hoteli ya Tansome mshtakiwa huyo Lilian alimsaidia  Joyce ambaye ni Ofisa Msaidizi wa Kodi wa TRA  kujipatia   Sh400,000 kutoka kwa Antelo Sanga  ili asiweze  kumpatia cheti cha faini cha VAT.

Baada ya kusomewa mashtaka hayo washtakiwa walikana na upande wa mashtaka ulidai kuwa upelelezi bado haujakamilika.

Hakimu Sachore  alimtaka kila mshtakiwa kuwa na wadhamini wawili wenye barua kutoka katika taasisi zinazotambulika kisheria  ambao watasaini ahadi ya Sh5 milioni kwa kila mmoja. Na kwamba barua hizo zitahakikiwa.

Kesi hiyo imeahirishwa hadi Machi 20, 2018 kwa ajili ya kutajwa ili kuangalia kama upelelezi utakuwa umekamilika au la.

Chapisha Maoni

0 Maoni